Saturday 27 April 2013

MBUNGE LEMA WA ARUSHA ASHIKILIWA NA POLISI KWA TUHUMA ZA UCHOCHEZI

Na Mahmoud Ahmad, Arusha
  Jeshi la polisi mkoani hapa limemtia mbaroni mbunge wa jimbo la Arusha mjini Mhe Godless Lema kwa tuhuma za uchochezi kwa wanafunzi kwenye chuo cha uhasibu mwanzoni mwa wiki katika vurugu zilizotokea chuoni hapo baada ya mwenzao kuuwawa juzi usiku huko maeneo ya njiro jijini hapa.
 
Kamanda wa polisi mkoani hapa kamishna msaidizi wa polisi Liberatus Sabas alisema kuwa Mhe Lema  alikamatwa huko nyumbani kwake Njiro majira ya saa 9 usiku. 
 
Afande  Sabas alisema jeshi hilo linaendelea na mahojiano na mtuhumiwa na kuwa katika tukio hilo zaidi ya watuhumiwa 14 walifikishwa mahakamani jana na kuwa hao hawezi kuwaongelea kwani kesi yao ipo kwenye chombo hicho cha sheria. 
 
 Pia kamanda Sabas alisema kuwa Mh Lema anashikiliwa kutokana na vurugu zilizotokea juzi kwenye chuo cha uhasibu na kuwa atafikishwa mahakamani siku ya jumatatu.
Kwa upande mwengine Kamanda Sabas  alisema kuwa zaidi ya hao watu 14 na Mhe. Lema hakuna mtuhumiwa mwingine aliyakamatwa. Awali ilisemakana wakili wake Albert Msando nae amekamatwa.
 
 Mnamo siku ya Jumatatu mwanafunzi mmoja aliuwawa kwenye mitaa ya Njiro jijini Arusha na watu wasiojulikana hali iliyoleta tafrani hadi wanafunzi hao walipoleta vurugu chuoni hapo na polisi kutumia mabomo ya machozi kuwatawanya.
 
Sekeseke hilo lilimalizwa na jeshi la polisi baada ya wanafunzi kutotii amri ya mkuu wa mkoa huo Magessa Mulongo na kuanza kuingia barabarani kuandamana.

No comments:

Post a Comment

TUPE MAONI YAKO