Wednesday 31 July 2013

Polisi waliohusika na ujangili wa meno ya tembo kizimbani

   POLISI wawili wa Kituo cha Polisi Oysterbay Dar es Salaam, Koplo Senga Idd (47) na Konstebo Issa Mtama (29) na wenzao saba waliokamatwa na vipande 70 vya meno ya tembo vyenye thamani ya Sh milioni 850,  walifikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili. Watu hao walikamatwa katika kizuizi cha Kauzeni, Kata ya Vikumbulu Tarafa ya Chole Kisarawe mkoani Pwani.


Watuhumiwa hao walifikishwa katika Mahakama ya Mkoa wa Pwani, wakiwa chini ya ulinzi mkali wa polisi.

Hata hivyo walibainika kukabiliwa na mashtaka mawili ya kukutwa na nyara za serikali kinyume na sheria na kuhujumu uchumi.

Akisoma mashtaka hayo, Wakili wa Serikali, Cecilia Shelly alidai mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mkoa wa Pwani, Bahati Ndeserua alidai washtakiwa walitenda kosa hilo Julai 28 mwaka huu wilayani Kisarawe.

"Watuhumiwa wanashtakiwa wote kwa pamoja kwa kumiliki nyara za serikali vipande 70 vya meno ya tembo bila kibali cha Mkurugenzi wa Wanyamapori,'' alidai Shelly.

Hakimu Ndeserua alisema washtakiwa hawatakiwi kutoa utetezi wowote katika mahakama hiyo kwa vile kesi hiyo inapaswa kusikilizwa katika Mahakama Kuu.

Alisema pia kuwa mahakama hiyo haina uwezo wa kutoa dhamana kwa washtakiwa hao.

"Washtakiwa nadhani wote mmesikia makosa yenu, hivyo mahakama hii haitaweza kuwapa nafasi ya kujibu lolote kwa sababu mamlaka makubwa ya kesi yapo Mahakama Kuu.

“Hii imetokana na kesi yenu kuwa ya kuhujumu uchumi na kukutwa na nyara za serikali kinyume na sheria,'' alisema Ndeserua.

Wengine waliopandishwa kizimbani ni Hamidu Salumu (35), mkazi wa Yombo njia Panda ambaye alikuwa dereva wa gari lililobeba meno hayo aina ya Toyota Surf.

Prospa Maleto (36) wa Tandika Dar es Salaam, Seif Kadro (35) wa Panga la Mwingereza Kata ya Vikumbulu wilayani Kisarawe, Ramadhani Athumani (45) wa Chanika Dar es Salaam nao walifikishwa kortini.

Wengine ni Musa Ally (35) mkazi wa Kinondoni Studio Dar es Salaam, Said Mdumuka (28) wa Panga la Mwingereza Chole wilayani Kisarawe Mkoa wa Pwani na Amri Bakari (33) wa Charambe Mbagala Dar es Salaam.

Watuhumiwa wote walirudishwa rumande na kesi hiyo itatajwa tena Agosti 14 mwaka huu

"NIPO TAYARI KUPIGWA RISASI KAMA ITATHIBITIKA NINAHUSIKA NA MADAWA YA KULEVYA "....MBUNGE AZZAN



Wakati Jeshi la Polisi likitoa visingizio kwamba linashindwa kunasa watuhumiwa wanaosafirisha dawa za kulevya wanaopitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), kutokana na kukosekana kwa vitendea kazi, Mbunge wa Kinondoni (CCM), Idd Azzan, amesema yupo tayari kupigwa risasi au kunyongwa hadharani kama itathibitika anahusika na biashara hiyo.

Azzan alitoa kauli hiyo jana wakati akihojiwa na kipindi cha Kumepambazuka kinachorushwa na Radio One kuhusu kuwapo kwa madai ya barua iliyoandikwa na Mtanzania aliyefugwa Hong Kong nchini China akimtaja kuhusika na biashara ya dawa hizo.

Alisema hahusiki kwa namna yoyote ile na biashara ya dawa za kulevya au biashara yoyote haramu na kwamba taarifa zilizoandikwa kwenye mitandao ya kijamii ni za upotoshaji na zimetolewa kwa lengo la kumchafua.

 “Nimejipeleka polisi kwa mara nyingine tena na nimewaomba wafanye uchunguzi wa kina na kama nitabainika nahusika na biashara hiyo niko tayari kupigwa risasi hadharani, lakini pia sitendewi haki kwa wale ambao wanazusha jambo hili wachukuliwe hatua za kisheria,” alisema. 



Azzan aliongeza kuwa hayupo juu ya sheria hivyo ikithibitika kuna mtu anamtuma dawa za kulevya kupitia bandari fulani pia atakuwa tayari kuwekwa hadharani na kunyongwa maana atakuwa hafai kuendelea kuwapo Tanzania.

Alisema makundi yanayomwandama ni ya kisiasa kwa lengo la kutaka kumdhoofisha katika kipindi cha kuelekea uchaguzi mkuu wa 2015.

Mahojiano kati ya Azzan na radio yalikuwa kama ifuatavyo;

RADIO: Mhe Idd Azzan wewe ni mbunge wa Kinondoni inaelezwa kuwa wewe ni mmoja kati ya watu wanaojihusisha na dawa za kulevya na mmekuwa mkipokea mizigo kupitia maboti makubwa yanayotoka Pakistan yanayopitia Bagamoyo, Tanga, Mtwara na Dar es Salaam, hebu tujuze na wajuze Watanzania hili lina ukweli gani.

AZZAN: Hata mimi nimesikia hilo na bahati nzuri nimesoma kwenye mitandao kadhaa imeandika hivyo na kuna barua inayodaiwa kuandikwa na mfungwa mmoja ambaye amedai mimi ndiye nahusika kumtuma yeye.
 


 Napenda kuwajulisha Watanzania sihusiki kwa namna yoyote ile na biashara ya dawa za kulevya na siyo dawa za kulevya tu lakini pia biashara yoyote haramu sijawahi kufanya katika maisha yangu.

Niseme tu kuwa hizo ni taarifa ambazo zimetolewa kwenye mitandao ili kuaminisha watu hivyo, lakini kimsingi sihusiki na sijihusishi na biashara ya namna hiyo.

Baada ya kuziona habari hizi kwenye mitandao nilichokifanya na sababu ilishawahi kujitokeza tena na viongozi wangu wa CCM walishawahi kuyasema hayo kwenye mkutano wa vijana nikawaambia polisi wachunguze ili kupata ukweli wa hilo jambo.

Kama itabainika nahusika basi nichukuliwe hatua za kisheria mimi siyo Mungu wala sipo juu ya sheria, nimefanya hivyo kwa maana ya kuongea na Jeshi la Polisi nimejipeleka nimetoa maelezo na nimewataka polisi kwa sababu ni kazi yao wafanye uchunguzi wa kina, pili kama nahusika na tuhuma hizo hatua za kisheria zifuatwe dhidi yangu na kama siyo kweli hao wanaoeneza uzushi huo pia wachukuliwe hatua.

 RADIO: Unadhani kwa nini Mtanzania aliyeshikiliwa Hong Kong amekutaja wewe kuhusika na biashara hiyo?

AZZAN: Kwanza mimi siamini kwamba kuna Mtanzania anayeshikiliwa Hong Kong ambaye amenitaja mimi, sababu hiyo biashara kwanza sijawahi kuifanya, mimi niliiona hiyo barua haina jina la huyo Mtanzania mnayemsema, wala hakuna namba ya mfugwa sasa mfungwa anatakiwa kuwa na namba, asitaje jina ataje basi walau namba yake pia hakuna jina la gereza, kwa hiyo mimi siamini Mtanzania ambaye amefugwa kwa tuhuma za dawa za kulevya anitaje mimi kuwa nimemtuma. Hakuna hicho kitu na hakuna Mtanzania ambaye niliwahi kumtuma hicho kitu kimetengenezwa kwa nia ya kunichafua.

RADIO: Mheshimiwa unatafsiri vipi tukio hili?

AZZAN: Mimi ninachotafsiri tayari mapambano ya 2015 ndiyo yanaanza na watu wanatafuta jinsi ya kunichafua sababu hata tukienda kwenye kura nitawashinda, lakini si kutafuta mbinu chafu za kunichafua.

Yapo maneno ambayo nayazungumza bungeni hayawafurahishi wengine, lakini kwa Watanzania wengi yana manufaa, kwa hiyo kwa wale ambao hayawafurahishi wanaweza wakawa wamechangia katika kunichafua.

RADIO: Lakini Mheshimiwa Idd Azzan mara nyingi tu umekuwa ukitajwa na watu mbalimbali kwamba unajihusisha na uuzaji wa dawa za kulevya ama wewe ni mmoja kati ya watu wanaowaagiza watu mbalimbali kusafirisha mizigo hiyo ya dawa za kulevya hilo kwa upande wako unalizungumza vipi.

AZZAN: Nasema binafsi nimejipeleka polisi na nilishajipeleka mara ya kwanza baada ya kutokea tuhuma kama hizi, nikawaambia polisi wafanye uchunguzi kama nahusika nichukuliwe hatua za kisheria, nimekwenda tena kuwaambia polisi na nasisitiza polisi wafanye uchunguzi wa kina kama nahusika hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yangu.

Kama nitabainika nahusika na biashara hiyo niko tayari kupigwa risasi hadharani, lakini pia sitendewi haki kwa wale ambao wanazusha jambo hili wachukuliwe hatua za kisheria.

RADIO: Lakini Mheshimiwa kwa upande mwingine tayari taarifa zimeshatolewa kama hivyo kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii, sasa endapo itabainika kweli umehusika ama hujahusika ni kitu gani ambacho utakifanya.

AZZAN:  Naomba niweke wazi kama itathibitika ninamtuma mtu madawa ya kulevya kupitia bandari gani mimi nipo tayari kuhukumiwa sababu sipo juu ya sheria na pia nipo tayari niwekwe hadharani waninyonge sifai kuendelea kuwapo Tanzania kama nahusika na hilo, na kama sihusiki serikali initendee haki kwa watu wanaosambaza uvumi huu nao wachukuliwe hatua siyo wakae tu na kumrushia mtu vitu vya uongo.

Awali Kamanda wa Polisi Viwanja vya Ndege, Deusdedit Kato akihojiwa katika kipindi hicho juu kwanini JNIA umeonekana kuwa kitovu cha kupitishia dawa za kulevya, alisema sababu kubwa ni kwamba kuna tofauti kati ya nchi na nchi katika masuala ya teknolojia katika kubaini dawa za kulevya.

Kamanda Kato alisema nchi nyingine wana vifaa vya kisasa zaidi na kwamba wakati sasa umefika kwa serikali kuwekeza katika kupata vitendea kazi zaidi ili kufanikisha mapambano ya dawa za kulevya.

Aliongeza kuwa wamekuwa wakishirikiana na viwanja vingine vya nchi mbalimbali kwa kubadilishana taarifa lengo likiwa ni mapambano ya biashara hiyo.

“Kimsingi wanaokamatwa wanakuwa ni wabebaji tu na siyo matajiri wa dawa za kulevya, bahati mbaya wabebaji wamekuwa wagumu sana kutoa ushirikiano kwa polisi, nasisitiza vitendea kazi vinachangia kuponya mtu asikamatwe nchini na kwenda kukamatwa nje,” alisema.

 Kamanda Kato alisema katika kipindi cha miezi sita hadi nane watu 14 wamekamatwa wakituhumiwa kusafirisha dawa za kulevya nchini.

•Julai 5, mwaka huu wasichana wawili, Agnes Jerald (25) na Melisa Edward (24), walipita JNIA na shehena ya dawa za kulevya kilo 150  na walikamatwa Afrika Kusini na kushtakiwa nchini humo kwa tuhuma za kukutwa na dawa za kulevya.
 

Hawa walikamatwa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Oliver Tambo wakiwa na shehena ya dawa hizo aina ya Crystal Methamphetamine zenye thamani ya zaidi ya Sh. bilioni 6.8.

•Ijumaa wiki iliyopita yaani Julai 26, mwaka huu, Watanzania wengine wawili, walikamatwa Hong Kong wakiwa na dawa za kulevya aina ya cocaine na heroine zenye thamani ya Sh. bilioni 7.6 akiwamo mmoja aliyekamatwa akitokea Dar es Salaam kupitia Dubai hadi Hong Kong.

Taarifa kutoka Hong Kong za Ijumaa wiki iliyopita zinaeleza kwamba, maofisa ushuru wa Uwanja wa Ndege wa Hong Kong (HKIA), walimkamata kijana mmoja mwenye umri wa miaka 26 akitokea Tanzania na alikuwa na dawa za kulevya aina ya heroine kilo 1.6 zenye thamani ya Sh. bilioni 1.5, kwenye mzigo wake wa mkononi.

•Siku hiyo hiyo jioni, maofisa hao walimkamata Mtanzania mwingine mwenye miaka 45 ambaye alipelekwa hospitali na kutolewa gramu 240 za dawa za kulevya aina ya heroine. Taarifa zaidi zilieleza kuwa Mtanzania mwingine mwenye miaka 28 alikamatwa akiwa na kilo 2.03 za cocaine.



Source: Nipashe.

Tuesday 30 July 2013

KESI YA LADY JAYDEE YAPIGWA KALENDA



MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kinondoni, leo imeiaharisha kesi inayomkabili msanii wa kizazi kipya nchini, Judith Wambura 'Lady Jaydee' a.k.a Annaconda dhidi ya uongozi wa Clouds Media Group hadi Agosti 2, mwaka huu.

Kesi hiyo ya madai iliyopo mbele ya Hakimu Athumani Nyamlani, leo ililetwa kwa ajili ya kusikilizwa lakini ilishindikana kutokana na wakili anayemtetea, Jaydee kutotokea mahakamani hapo na kumtuma mwakilishi wake.

Ilidaiwa mahakamani hapo kuwa wakili huyo wa Jaydee, amekwenda katika Mahakama Kuu kuhudhuria kesi nyingine na hivyo kushindwa kufika mahakamani hapo kuendelea na kesi hiyo na hivyo kuahirishwa hadi Agosti 2, mwaka huu.

Kesi hiyo ya madai ilipelekwa mahakamani hapo na Mkurugenzi wa Utafiti na Maendeleo wa Kampuni ya Clouds Media kwa madai ya kuukashifu uongozi huo.


 Kwa mujibu wa mdai huyo, ambaye ni uongozi wa Clouds Media ulidai kuwa mdaiwa huyo ambaye ni Lady Jaydee aliandika maneno ya kuukashifu uongozi huo kupitia blogu yake.

MKUU WA WILAYA YA TUNDURU NALICHO AWATIMUA WAVAMIZI MSITU WA SHAMBA LA BIBI

Na Steven Augustino, Tunduru

MWENYEKITI wa kamati ya Ulinzi ya Wilaya ya Tunduru, Mkuu wa Wilaya hiyo Mkoani Ruvuma Chande Nalicho ametoa wiki moja kwa Wakulima na Wafugaji wa jamii ya Kisukuma kuondoka katika eneo la hifadhi ya msitu wa Shamba la Bibi vinginevyo hatua kali za Kisheria zitachukuliwa dhidi yao.
 
Dc, Nalicho alitoa maagizo hayo baada ya kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya hiyo kufanya ziara ya kushtukiza katika msitu huo na kujionea hali halisi ya uhalibifu wa vyanzo vya maji, mabwawa na misitu iliyopo katika hifadhi hiyo inayo unganisha Vijiji vya Nangunguru, Majala na Mkalekawana katika Tarafa ya Nampungu kata ya Nandenbo Wilayani humo.
 
Alisema anatoa siku Saba kwa watu wote waliovamia msitu huo wa hifadhi kuondoka kwani haiwezekani watu waendelee kuishi wanavyo penda na kuharibu mazingira katika vyanzo vya maji na hifadhi ya misitu kana kwamba serikali haipo
 
Mkuu huyo aliwataka Watendaji Kata ,Vijiji kwa kushirikiana na Maafisa Tarafa Wilayani humo kutekeleza majukumu yao ikiwemo kuwaelekeza wafugaji kufuata taratibu za kuonana na viongozi wa Vijiji husika, kufanya mikutano inayo wahusisha wananchi katika maamuzi ya kuwapokea wafugaji hao ili kuyaondoa maeneo yao katika migogoro ya aina hiyo.
 
“Kwavile mifugo ni muhimu kwetu na endapo itatumika vizuri na kwa kuzingatia kanuni, miongozo na maelekezo yanayotolewa na Serikali italeta manufaa kwa Wananchi wetu” alisema Dc, Nalicho na kuongeza kuwa mtindo wa kuishi kwa uhasama kati ya wafugaji na wakulima hauwezi kuwa na tija.
 
Awali akiongea katika ziara hiyo Afisa misitu wa Wilaya la Tunduru  Rashid Mtotela alimweleza Dc, Nalicho kuwa Wakulima na wafugaji hao walivamia msitu huo mwaka 2006 /2007 na kuendelea kujiimarisha kila mwaka baada ya kubaini kutokuwepo kwa vikwazo vyovyote kutoka Serikalini.
 
Alisema hifadhi hiyo ambayo awali ilikuwa imeunganishwa na Hifadhi ya Taifa (Selous) tangu mwaka 1974 na baadae kuunda hifadhi shirikishi mwaka 2007 kupitia mradi wa Jont participatory Forest Menegement (JPFM) liyounganisha Vijiji vya Nangunguru, Mkalekawana na Majala kila Kijiji kimekuwa kikikwepa majukumu yake ya kulinda hifadhi hiyo hali ambayo imechangia kuendelea kuhalibika kwa mazingira hayo.
 
Wakiongea kwaniaba ya Wananchi wa Vijiji hivyo Mwenyekiti wa Kijiji cha Nangunguru Bw.Said Rashid Mkwekwele, Mtendaji wa Kijiji hicho Zainabu Twaha na Afisa Tarafa wa Nampungu Joshua John wakawashushia lawama baadhi ya wakuu wa Idara katika halmashauri ya Wilaya hiyo kuwa umekuwa na kigugumizi katika ufuatiliaji na uchukuzi wa maamuzi juu ya migogoro hiyo.

TASWIRA YA WEMA KATIKA MFUNGO WA RAMADHANI

Monday 29 July 2013

WAANDISHI WAPATA TUZO YA USALAMA WA BARABARA

Marwa Press 26.07.2013 009 
 Mkurugenzi msaidizi wa Idara ya Habari maelezo Bi. Zamaradi Kawawa akionyesha tuzo aliyoipokea kwa niaba ya Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo Bw.Assa Mwambene  iliyotolewa na Automobile Association of Tanzania kwa waandishi wa habari walishiriki katika kutoa taarifa kwa wananchi kuhusu matumizi mazuri ya  barabarani.
Marwa Press 26.07.2013 016 
 Rais wa Automobile Association of Tanzania Bw.Nizar Jivani kulia, akitoa tuzo kwa bw. Abdilahi Kombo ambaye ni mratibu wa AAT kwa ushiriki mzuri wa kutoa taarifa kwa wananchi kuhusu matumizi mazuri ya barabara.
Marwa Press 26.07.2013 020 
 Bw. Judica Benedict mwandishi wa habari wa gazeti la  The Guardian kushoto akipokea tuzo kutoka kwa Rais wa Automobile Association of Tanzania Nizar Jivani kwa ushiriki mzuri wa kutoa taarifa kwa wananchi kuhusu matumizi mazuri ya barabara.
Marwa Press 26.07.2013 024  
Bw.Fredy Mwanjala mwandishi wa habari wa gazeti la Mwananchi kushoto akipokea tuzo kutoka kwa Rais wa Automobile Association of Tanzania Nizar Jivani  kwa ushiriki mzuri wa kutoa taarifa kwa wananchi kuhusu matumizi mazuri ya barabara
Marwa Press 26.07.2013 027 
Rais wa Automobile Association of Tanzania Nizar Jivani (wa tano kutoka kushoto waliosimama)  akiwa katika picha ya pamoja na waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali vya habari baada ya kupokea tuzo ya ushirikiano wa kutoa taarifa kwa wananchi kuhusu matumizi mazuri ya barabara,(picha zote na Lorietha Laurence-maelazo)
Na Jennifer Chamila, MAELEZO.
 TAASISI ya Automobile Association Tanzania (AAT) imetoa tuzo kwa waandishi wa habari kutoka katika  vyombo vya mbalimbali vya habari walio shiriki katika kutoa habari kwa wananchi kuhusu mafunzo yalio tolewa kwa waendesha bajaji na pikipiki  2500 kuhusu matumizi salama ya barabara.
Tuzo hizo zimetolewa leo  pamoja fedha taslimu na Rais wa taasisi hiyo Bw.Nizar Jivan katika sherehe fupi ilio fanyika ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO) jijini Dar es Salaam,Waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali vya habari wamewaza kujinyakulia tuzo hizo.
 Rais  huyo alitoa tuzo  hizo  kwa waandishi na watu waliosaidia kukamilisha mafunzo hayo, ambapo    miongoni mwao ni Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo Bw.Assa Mwambene, ambaye tuzo yake ilikabidhiwa kwa Mkurugenzi Msaidizi wa Idara hiyo, Zamaradi  Kawawa. 
 
Wengine waliopata tuzo hizo ni Mohamed Ugassa kutoka gazeti la The Guardian,Freginia Ole Swai kutoka ITV,Fred Mwanjara wa Channel Ten,Elias Shamt wa TBC,Miguel Suleiman wa Citizen,Nasongelya Kilyanga wa Daily News,Khadija Mussa wa gazeti wa Uhuru,Zainabu Malongo kutoka Mwananchi,Hadja Hamis kutoka Mtanzania,Abas Yusuph mwandishi wa kujitegemea,Judica Benedict wa The Guardian.
 
Akizungumza na waandishi wa habari katika sherehe hiyo Bw.Nizar amesema kuwa,anawashukuru waandishi wa habari kwa kusaidia kutoa habari kwa wananchi juu ya mafunzo hayo yalio husisha matumizi salama ya barabara na jinsi ya kuepusha ajali za barabarani.
 
Vilevile taasisi hiyo imeitaka Serikali kuweka mikakati madhubuti ambayo itarahisisha kupambana na matumizi mabaya ya barabara.
 
“Serikali ihakikishe bodaboda zote zipewe namba maalumu ili iwe rahisi huzitambua pindi uhalifu utakapotokea kama ilivyo kwa teksi,” alisema Jivan.
 
Naye mmoja wa waandishi wa habari aliyejinyakulia tuzo hizo , Ugassa kutoka gazeti la The Guardian,ametoa wito kwa waandishi wa habari kuzidisha uhamasishaji  dhidi ya  matumizi bora ya barabara na kulipa mkazo suala hilo kama wafanyavyo katika masuala mengine kama vile Ukimwi.

RAIS KIKWETE ATAWAZWA OMUKAMA (CHIFU) WA MISSENYI, AHITIMISHA ZIARA YA KAGERA

bk7Rais Jakaya Kikwete akitawazwa kuwa Omukama (Chifu) wa Missenyi wakati wa ziara yake ya siku sita mkoani Kagera. Anayemsimika ni kiongozi wa wazee wa Missenyi, Mzee Ernest Babeiya.
bk6bk1Rais Jakaya Mrisho Kikwete akihutubia maelefu ya wananchi wa mkoa wa Kagera waliofurika katika uwanja wa michezo wa Kaitaba kumsikiliza siku ya mwisho ya ziara yake ya siku sita mkoani humo.PICHA NA IKULU

TBC SONGEA WAMNYONYOA JOGOO FM 6 KWA 1

 Toka kulia ni Issa Rashidi aliye wanyonyoa bao 4, katikati ni Tamimu Adamu mchezaji wa Jogoo Fm na wa mwisho ni Hamza Juma
 Baada ya Issa Rashidi kuwanyonyoaa 4 bila uluma shabiki wa Jogoo akaamua kupiga picha na mnyonyoaji wa TBC
 Hakika Jogoo hawata msahau Issa Rashidi
 Hawa ni wachezaji wa TBC Songea
 Gerson Msigwa akitoa maelezo na namna ya kumnyonyoa Jogoo FM pia nae akawanyonyoa Moja
Toka kushoto ni mwakilishi wa ITV Songea Nathan Mtega , Hanna Mayige mkuu wa kanda (TBC Songea) na Good mfanyakazi wa TBC wakiangalia mchezo katika uwanja wa Sokoine
Hapa ilikuwa ni kabla ya mchezo kuanza toka kulia ni Mathew Chisala, Issa Rashidi, Shekhan Mzaina,Rauph Mohamed na Hamza Juma
VIA/demashonews

Sunday 28 July 2013

MDAU SIMALENGA WA CLOUDS FM AKUBALI YAISHE,AFUNGA NDOA NA NEEMA INANA .


Kambi ya Wasanii wa Filamu na Maigizo pamoja na Kambi ya Wanahabari Makapela Tanzania imepata pigo kubwa baada ya Mwanachama wake Nguli, Simon Simalenga kuamua kuiaga kambi hiyo na kuingia rasmi katika Kambi Tawala ya Wanandoa baada ya kufunga Ndoa na Bi. Neema Inana.

Wawili hao wameamua kuingia kambi hiyo ya Upinzani katika mahusiano leo katika Kanisa Katoliki Parokia ya Bikira Maria Mama wa Mwokozi Sinza jijini Dar es Salaam na baadae katika tafrija kubwa inayofanyika usiku huu wa Julai 27, 2013 katika ukumbi qa Grande Hall uliopo ndani ya Hoteli ya Picolo Beach Mbezi. 


TANZANIA YATOLEWA MICHUANO YA CHAN

Tanzania (Taifa Stars) imeshindwa kufuzu Fainali za Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN) kwa mara ya pili mfululizo baada ya jana(Julai 27 mwaka huu) kufungwa mabao 3-1 na Uganda Cranes, hivyo kutolewa kwa jumla ya mabao 4-1.

Stars ambayo ilicheza fainali za kwanza zilizofanyika Ivory Coast mwaka 2009 ilimaliza kipindi cha kwanza katika mechi hiyo iliyochezwa Uwanja wa Taifa wa Mandela ulioko Namboole nje kidogo ya Kampala ikiwa sare ya bao 1-1.

Wenyeji ndiyo walioanza kufunga bao dakika ya saba katika mechi hiyo iliyochezeshwa na Kanoso Abdoul Ohabee kutoka Madagascar. Frank Kalanda alifunga bao hilo akimalizia mpira uliopigwa ndani ya eneo la hatari la Tanzania.

Bao hilo halikuonekana kuichangaza Taifa Stars, kwani ilitulia na kufanikiwa kusawazisha dakika ya 18 mfungaji akiwa Amri Kiemba kutokana na pasi nzuri ya Mrisho Ngasa kwenye kona ya eneo la mita 18.

Dakika ya 32 nusura Taifa Stars ipate bao, lakini mkwaju maridadi wa Mrisho Ngasa ambao tayari ulikuwa umempira kipa HAmza Muwonge uligonga mwamba kabla ya kuokolewa na mabeki wa Uganda Cranes.

Mabao mengine ya Uganda Cranes yalifungwa dakika ya 48 kupitia kwa Brian Majwega na lingine dakika ya 63 mfungaji akiwa tenda Kalanda kutokana na makosa ya Salum Abubakar kupokonywa mpira wakati akiwa katika nafasi nzuri ya kutoa pasi kwa mwenzake.

Kocha Kim Poulsen alifanya mabadiliko dakika ya 43 kwa kumuingiza Simon Msuva badala ya Frank Domayo aliyeumia, na dakika ya 78 akawaingiza kwa mpigo Haruni Chanongo na Vincent Barnabas badala ya David Luhende na John Bocco. Hata hivyo mabadiliko hayo hayakubadili matokeo ya mchezo.
Kikosi cha Stars kilipangwa hivi; Juma Kaseja, Erasto Nyoni, David Luhende/Vincent Barnabas, Aggrey Morris, Kelvin Yondani, Athuman Idd, Frank Domayo/Simon Msuva, Salum Abubakar, John Bocco/Haruni Chanongo, Amri Kiemba na Mrisho Ngasa.

Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager itarejea nyumbani kesho (Julai 28 mwaka huu) saa 4 usiku kwa ndege ya Precision Air.


Taswira Kutoka Chuo cha Polisi Moshi(CCP):Ona Jinsi Jeshi la Polisi Lilivyo imara


  MHITIMU WA MAFUNZO YA AWALI YA ASKARI POLISI AKIVUNJA VIGAE KWA KUPIGA NGUMI LEO MJINI MOSHI ALIPOKUA AKIFANYA ONYESHO LA UKAKAMAVU WAKATI WA SHEREHE ZA KUFUNGA MAFUNZO YALIYOJUMUISHA ASKARI POLISI NA UHAMIAJI. TAKRIBANI ASKARI POLISI ELFU TATU NA TISINI NA MBILI WALIHITIMU MAFUNZO, WAKIWEMO ASKARI WA UHAMIAJI HAMSINI NA MOJA KATIKA CHUO CHA POLISI MOSHI (CCP).
  MHITIMU WA MAFUNZO YA AWALI YA ASKARI POLISI AKIJIANDAA KUVUNJA VIGAE KWA KUPIGA NGUMI LEO MJINI MOSHI ALIPOKUA AKIFANYA ONYESHO LA UKAKAMAVU WAKATI WA SHEREHE ZA KUFUNGA MAFUNZO YALIYOJUMUISHA ASKARI POLISI NA UHAMIAJI. TAKRIBANI ASKARI POLISI ELFU TATU NA TISINI NA MBILI WALIHITIMU MAFUNZO, WAKIWEMO ASKARI WA UHAMIAJI HAMSINI NA MOJA KATIKA CHUO CHA POLISI MOSHI (CCP).
Wahitimu wa mafunzo ya awali ya askari polisi wakifanya onyesho la kareti  jana mjini moshi  wakati wa sherehe za kufunga mafunzo yaliyojumuisha askari polisi na uhamiaji. takribani askari polisi elfu tatu na tisini na mbili walihitimu mafunzo, wakiwemo askari wa uhamiaji hamsini na moja katika chuo cha polisi moshi (ccp).
 KIKUNDI CHA KARETI NA JUDO CHA WAHITIMU WA MAFUZO YA AWALI YA ASKARI POLISI NA UHAMIAJI WAKIFANYA ONYESHO LA KARETI KWA MGENI RASMI MH, Dr. EMMANUEL NCHIMBI WAKATI WA SHEREHE ZA KUFUNGA MAFUNZO HAYO. TAKRIBANI ASKARI POLISI ELFU TATU NA TISINI NA MBILI WALIHITIMU MAFUNZO, WAKIWEMO ASKARI WA UHAMIAJI HAMSINI NA MOJA KATIKA CHUO CHA POLISI MOSHI (CCP).
Askari polisi waliohitimu mafunzo, wakionyesha pikipiki inavyoweza kusaidia katika kukabiliana na wahalifu kwa waziri wa mambo ya ndani ya nchi mh, dr. Emmanuel nchimbi aliyekua mgeni rasmi katika sherehe za kufunga mafunzo ya awali kwa askari polisi na uhamiaji jana mjini moshi. takribani askari polisi elfu tatu na tisini na mbili walihitimu mafunzo, wakiwemo askari wa uhamiaji hamsini na moja.Picha na Hassan Mndeme-Jeshi la Polisi.
--
 Zaidi ya Askari Polisi wapya 3,092 wamehitimu mafunzo yao ya awali ya Polisi katika Chuo cha Polisi (CCP) kilichopo mjini Moshi mkoani Kilimanjaro.
Polisi hao wapya ambao wanaingia mtaani nchi nzima wataingia mtaani wakati wowote kuhakikisha ulinzi wa raia na mali zao unakuwa madhubuti.
Mafunzo yao yamefungwa chuoni hapo na Waziri Mwenye dhamana ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi kwa kushuhudia maonesho mbalimbali ya vitu walivyo jifunza jambo ambalo endapo kama watalitumia vyema basi litaleta chachu katika kukabiliana na uhalifu unao tikisa katika maeneo mbalimbali ya nchi pamoja na watu wasio tii sharia hadi washurutishwe.

Saturday 27 July 2013

RAY C ATANGAZA KURUDI UPYA KWENYE GAME LA MUZIKI.....



 
 Mabibi na mabwana mko tayari kwa ujio mwingine wa Ray- C. Malkia wa kiuno bila mfupa Rehema Chalamila aka Ray-C ametangaza ujio wake rasmi baada ya kuwa chimbo kwa kipindi kirefu toka apate matatizo miezi kadhaa iliyopita.
 
Ni baada ya siku chache kupita toka Ray-C atamke kuwa anapenda sauti ya ‘dogo lake’ Recho na kuwa atakuja kufanya naye kazi, leo amethibitisha kuwa mwezi Agosti ndio anarudi rasmi kutoka chimboni.

 
 Kupitia akaunti ya Instagram Ray-C aliweka picha ya gazeti moja lililoandika ‘Ray-C kuonekana hadharani mwezi Agosti’, na baada ya followers wake kutaka ufafanuzi ndipo alifunguka kwa kusema “For Sure it’s bout time nw nimewapa muda sana watoto sasa mdada is coming back”.

 
 Ray C aliwauliza marafiki zake wa Instagram kama wapo tayari kwa ‘come back’ yake, wengi wameonekana kutamani muda ufike waweze kumuona tena Ray-C akirudi katika muziki. Hizi ni baadhi ya comments kutoka kwa mashabiki wake.

TAIFA STARS KUSHAMBULIA MWANZO MWISHO

 
Moja ya mikakati ya Taifa Stars kwenye mechi ya leo (Julai 27 mwaka huu) dhidi ya Uganda kuwania kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Tatu za Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN) zitakazofanyika mwakani nchini Afrika Kusini ni kushambulia kwa muda mwingi wa mchezo.

Kocha Kim Poulsen amesema maandalizi ya Taifa Stars jijini Mwanza kwa ajili ya mechi hiyo ambayo Uganda inaongoza kwa bao 1-0 yalikuwa mazuri, lakini mabao ni muhimu hivyo watashambulia bila kusahau kulinda lango lao.

“Unapocheza mechi za aina hii za nyumbani na ugenini, huku mwenyeji akiwa anaongoza mabao yana maana kubwa katika mechi. Mabao yanabadili mchezo na pia wachezaji kifikra,” amesema Kim akizungumza na waandishi wa habari kwenye hoteli ya Mt. Zion ambayo Stars imefikia.

Amesema katika mechi ya kwanza walitengeneza nafasi nyingi lakini hawakuzitumia, hivyo wamekuwa wakifanya mazoezi ya kushambulia, jinsi ya kutengeneza nafasi, na jinsi ya kumalizia.

“Hivyo tuko hapa (Kampala) kwa ajili ya kufunga, ni lazima tufunge ili tuweze kuendelea na mashindano. Lakini ngome yetu nayo ni lazima iwe makini ili kutoruhusu bao,” amesema Kim na kuongeza kuwa kikosi chake cha kwanza ni lazima kitakuwa mabadiliko kutoka na Mwinyi Kazimoto kuingia mitini na Shomari Kapombe kwenda kwenye majaribio Uholanzi.

Amesema angalau kutakuwa na mabadiliko kwa kuingiza sura mbili mpya katika kikosi cha kwanza, na kuongeza kuwa wachezaji wanafahamu umuhimu wa mechi hiyo kwani timu ikienda kwenye Fainali za CHAN itakuwa manufaa kwao binafsi.

Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager imefanya mazoezi ya mwisho leo jioni Uwanja wa Mandela ulioko Namboole ambao utatumika kwa ajili ya mechi hiyo kesho.

Mechi hiyo itaanza saa 10 kamili jioni kwa saa za Afrika Mashariki na itachezeshwa na waamuzi kutoka Madagascar wakiongozwa na Kanoso Abdoul Ohabee wakati mwamuzi msaidizi namba moja ni Andirvoavonjy Pierre Jean Eric. Mwamuzi msaidizi namba mbili ni Jinoro Velomanana Ferdinand huku Andriamiharisoa Hubert Marie Bruno akiwa mwamuzi wa mezani (fourth official). Kamishna wa mechi hiyo namba 38 ni Ismail Kamal kutoka Ethiopia.

Stars inatarajiwa kupangwa hivi; Juma Kaseja, Erasto Nyoni, David Luhende, Aggrey Morris, Kelvin Yondani, Athuman Idd, Salum Abubakar, Frank Domayo, John Bocco, Amri Kiemba na Mrisho Ngasa.

MIYEYUSHO ASAINI MKATABA MPYA

                                                               

Thursday 25 July 2013

MWANAMKE ANYONGWA HUKO SHINYANGA BAADA YA MUMEWE KUMTUHUMU KUGAWA PENZI NJE YA NDOA YAO

Na Kadama Malunde, Shinyanga
 MWANAMKE mmoja Happiness Luhende mwenye umri wa miaka 28 mkazi wa Lubaga katika manispaa ya Shinyanga, ameuawa kwa kile kinachoelezwa kuwa ni kunyongwa na mume wake kwa kutumia kamba ya katani baada ya kumtuhumu kuwa anamsaliti kwa kufanya mapenzi na wanaumme wengine.

Tukio hilo limetokea juzi jioni majira ya saa 12 jioni katika kata ya Lubaga, ambapo watu walioshuhudia tukio hilo walisema Majija Clement mwenye umri wa miaka 22-23 ambaye ni mume wa marehemu aliona ujumbe mfupi kwenye simu ya mkewe uliokuwa unaashiria kuwa umetoka kwa mwanamme mwingine ukimtaka akutane naye eneo fulani, ndipo alipoamua kumpiga kisha kumnyonga kwa kutumia kamba ya katani.

Akizungumzia tukio hilo mjomba wa marehemu, John Sumari, alisema mpwa wake aliolewa mwezi 
Desemba mwaka jana na mpaka mauti yanamfika walikuwa hawajabahatika kupata mtoto.

“Marehemu ni mtoto wa dada yangu, wamekuwa wakigombana mara kwa mara, nimewahi kusuluhisha kesi mara mbili, kesi ya kwanza ilikuwa ni ya mwanamme kumtuhumu mke wake kuwa ana mwanamme mwingine baada ya kupigiwa simu. Kesi ya pili ilikuwa mwezi uliopita ambapo Majija Clement alimtuhumu mke wake kwamba anafanya mapenzi na balozi wa eneo hilo, lakini hayo yaliisha na leo ndiyo haya tena yametokea,” aliongeza.

Walioshuhudia tukio hilo walisema mtuhumiwa ni mwenyeji wa wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza na alikuja Shinyanga kwa mama yake na kubahatika kumwona Happiness akaanza kuishi naye kama mke wake. Alisema mwanaume huyo anafanya shughuli za kuchoma tofali na kuendesha baiskeli maarufu 'daladala'.

Mwenyekiti wa mtaa wa Lubaga, Shabani Mashishanga alisema mtuhumiwa alikuwa ni mhamiaji wa eneo hilo na ametoroka baada ya kufanya tukio hilo na jeshi la jadi (sungusungu) linamtafuta.

Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga, Kamishina Msaidizi wa Polisi, Evarist Mangalla alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kuwataka wananchi kuacha kujichukulia sheria mkononi huku akiwaomba kushirikiana na jeshi hilo kumtafuta mtuhumiwa ili sheria ichukue mkondo wake.

RAIS JAKAYA KIKWETE AZINDUA JENGO LA MAHAKAMA KUU KANDA YA BUKOBA


 Rais Jakaya Mrisho Kikwete akifungua pazia kuzindua rasmi jengo la Mahakama Kuu Kanda ya Bukoba leo Julai 25, 2013
 Rais Jakaya Mrisho Kikwete akikata utepe kuzindua rasmi jengo la Mahakama Kuu Kanda ya Bukoba leo Julai 25, 2013. Aliyeshika utepe ni Jaji Mkuu, Othman Chande
                     Rais Kikwete akiwa katika moja ya vyumba vya mahakama hiyo
             Rais Kikwete akifuatana na Jaji Mkuu wakati akikagua jengo la mahakama hiyo
 Jaji Mkuu Othman Chande akimpa maelezo Rais Kikwete wakati wakiwa kwenye jengo la mahakama hiyo.
 Rais Jakaya Kikwete na Jaji Mkuu wakiwa katika picha ya pamoja na viongozi wengine wa mahakama waliohudhuria uzinduzi wa jengo hilo la mahakama
Baadhi ya watu waliofika kwenye sherehe za uzinduzi wa jengo hilo. Picha na Ikulu

TUPE MAONI YAKO